Thursday, August 21, 2014

SHIRIKA LA MAGEREZA KUINGIA UBIA WA UCHIMBAJI MADINI YA CHOKAA NA KAMPUNI YA TWIGA CEMENT YA JIJINI DAR

Kamishna Jenerali wa Jeshi Magereza John Casmir Minja(kushoto) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Twiga Cement, Bw. Alfonso Rodrudges(kulia) kabla ya kusaini Makubaliano ya ubia kati ya Shirika la Magereza na Kmapuni hiyo ya uchimbaji madini ya chokaa katika eneo la Gereza Wazo Hill leo Agosti 21, 2014 Jijini Dar es Salaam.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza John Casmir Minja(kushoto) akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Twiga Cement, Bw. Alfonso Rodrudges(kulia) wakisaini nyaraka muhimu za Makubaliano ya ubia katika mradi wa uchimbaji madini ya chokaa katika eneo la Gereza Wazo Hill.
Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja(kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Twiga Cement, Bw. Alfonso Rodrudges(kulia) wakibadilishana nyaraka muhimu za Makubaliano ya ubia kati ya Shirika la Magereza na Kampuni ya Twiga Cement katika mradi wa uchimbaji madini ya chokaa katika eneo la Gereza Wazo Hill Jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakishuhudia utiaji sahini wa Makubaliano ya ubia wa mradi wa uchimbaji madini ya Ujenzi katika Gereza Wazo Hill Jijini Dar es Salaam.
Maafisa Wandamizi wa Jeshi la Magereza walioshiriki hafla ya utilianaji sahini Makubaliano ya ubia huo wakimsikiliza Mtaalam Mshauri wa Kampuni ya Twiga Cement, Bw. Said Abdallah(hayupo pichani) namna Jeshi la Magereza litakavyonufaika na mradi huo wa madini.(Picha zote na Lucas Mboje wa Jeshi la Magereza).

Na; Lucas Mboje

Jeshi la Magereza nchini kupitia Shirika lake la Magereza limeingia makubaliano rasmi ya mradi wa uchimbaji madini ya Chokaa na Kampuni ya Saruji ya Twiga katika eneo la Gereza Wazo Hill Jijini Dar es Salam.

Makubaliano hayo yamefanyika leo Alhamisi 21 Agosti, 2014 katika Ukumbi wa Mkutano wa Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza pamoja na Wanahabari, Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, John Casmir Minja amesema kuwa ushirikiano huo kati ya Shirika la Magereza na Twiga Cement unalenga kuimarisha Shirika la Magereza ili liweze kujiendesha kibiashara kwa kuchangamkia fursa mbalimbali za kiuchumi.

Ametaja madini na maeneo ambayo Jeshi hilo litafanya uchimbaji madini kwa ubia ni pamoja na Chokaa, mawe, kokoto, mchanga, zahabu na moramu   katika maeneo ya Magereza mbalimbali hapa nchini ambayo ni Maweni(Tanga), Lilungu(Mtwara), Bahi(Dodoma), Msalato(Dodoma), Majimaji(Songea), Kalilankulukulu(Mpanda).

“Tayari Jeshi la Magereza limepata leseni 164 za Uchimbaji wa madini ya Ujenzi, vito na zahabu katika maeneo mbalimbali ya magereza hapa nchini” Alisema Kamanda Minja.

Kamishna Jenerali Minja ameongeza kuwa upatikanaji wa leseni hizo ni mojawapo ya hatua ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazolikabili Jeshi la Magereza, hususani katika kuipunguzia Serikali gharama za kuhudumia magereza na kuongeza pato la Kodi kwa Taifa.

“Vyanzo vilivyobuniwa kuongeza tija ni pamoja na kuingia ubia na Wawekezaji wenye nia ya dhati ya kushirikiana na Jeshi letu katika madini hayo” Alisisitiza Kamanda Minja.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Twiga Cement, Bw.Alfonso Rodrudges amesema kuwa Kampuni yake ipo tayari kwa dhati kushrikiana na Shirika la Magereza katika mradi huo wa uchimbaji madini ya ujenzi na kuwa yapo mahitaji makubwa ya bidhaa hiyo katika Ujenzi wa Barabara katika Jiji la Dar es Salaam.

“Makubaliano haya ya ubia yataongezea uhakika wa upatikanaji wa madini ya chokaa katika maeneo ya karibu na Kiwanda chetu hivyo kuongeza uzalishaji wa saruji nchini na kuwa na muda mrefu zaidi(lifespan) wa kuendesha shughuli za Kiwanda chetu” Alisema Bw. Rodrudges.

Pia ameongeza kuwa mbali na kuliongezea mapato Jeshi la Magereza katika mradi huo pia Kampuni yake itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za kuishi Maofisa na Askari wa Gereza Wazo Hill Jijini Dar es Salaam hivyo kupunguza changamoto kubwa ya uhaba wa nyumba za kuishi askari.

Mkakati wa Jeshi la Magereza hivi sasa ni kuendelea kuboresha maeneo mbalimbali pamoja na kuchangamkia fursa zilizopo ili kuhakikisha kuwa linafikia ufanisi unaotarajiwa katika utekelezaji wa majukumu yake.

Makubaliano hayo yatakuwa na manufaa makubwa kwa Shirika la Magereza katika kukuza mtaji na kubadilishana ujuzi katika miradi mbalimbali ya madini hayo.

No comments: