Thursday, February 26, 2015

Tamthilia ya "A Boys Mission" yahitaji Milioni 800 ili ikamilike

Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni ya Forward Formidable Enterprises (FFE) inayoandaa tamthilia mpya na ya kisasa ya “A boys mission” Johnson Lujwangana katikati akifafanua jambo kuhusiana na tamthilia hiyo itakayoanza kurushwa kwenye vituo vya televisheni kuanzia mwezi septemba. Wengine katika picha kutoka kushoto ni Brian daniel, Neema Mung'anya, Samuel katabazi, Jesca haule, Aisha bakari na Victor Casmir.
Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni ya Forward Formidable Enterprises (FFE) inayoandaa tamthilia mpya na ya kisasa ya “A boys mission” Johnson Lujwangana akifafanua jambo kuhusiana na tamthilia hiyo itakayoanza kurushwa kwenye vituo vya televisheni kuanzia mwezi septemba. Wengine katika picha kutoka kulia ni Jesca haule na Aisha bakari.
Waigizaji wa tamthilia ya “A boys mission” inayoandaliwa na kampuni ya Forward Formidable Enterprises katika picha ya pamoja.

Na Mwandishi wetu
Kampuni mpya katika utengenezaji wa filamu nchini, Forward Formidable Enterprises (FFE) inayoandaa tamthilia mpya na ya kisasa ya “A boys mission” inahitaji kiasi cha Sh milioni 800 ili ikamilike.

Mwenyekiti Mtendaji wa kampuni ya FFE, Johnson Lujwangana alisema kuwa kwa sasa wameweza kutengeneza toleo la utangulizi "pilot episode' kwa ajili ya kuonyesha nini wanakifanya huku kila kitu kikiwa tayari kwa ajili ya kurekodiwa.

Johnson alisema kuwa tamthilia yao inazungumzia changamoto na suluhisho mbalimbali kwa maisha ya vijana nchini na fedha hizo zinahitajika kwa ajili ya kughalimia gharama mbalimbali za kuzalisha rasmi tamthilia hiyo.

Baadhi ya gharama hizo kwa mujibu wa Johnson ni kulipa mtayarishaji bora, kuwalipa wasanii fedha kutokana na ubora wa kazi zao, kulipia vifaa vya kisasa, kulipa sehemu bora ya kurekodi tamthilia, usafiri, chakula na gharama nyinginezo.

“Kama msanii wa muziki wa kizazi kipya, Diamond anatengeneza video ya dakika tatu kwa Sh Milioni 60, kwa nini tamthilia ambayo kila sehemu (episode) inatumia si chini ya dakika 45 hisifikia kiwango hicho cha fedha? Alihoji Johnson.

Alisema kuwa wao wanataka kuwafaidisha wasanii wao kwa kuwalipa vizuri na kuendelea kudumu katika fani na kuwataka wadhamini kujitokeza kwa wingi kusaidia mradi huo.

“Hakuna hata msanii mmoja maarufu katika tamthilia hii, lengo si kama kuwatupa wasanii hao, bali ni kupanua wigo na kuwapa nafasi wasanii wengine, nataka kizazi kipya zaidi katika tasnia ili kuendeleza kuzalisha mastaa,” alisema.

Alisema kuwa katika tamthilia imeonyesha na kutoa majibu ya nini vijana wanatakiwa kufanya hapa nchini na kuachana na fikra za kukimbilia nje ya nchi  kwa kudhani kuwa ndiko kutakuwa suluhisho la matatizo yao.

Alifafanua kuwa mara baada ya kufika huko, hali inakuwa tofauti na kukutana na changamoto nyingi zaidi za maisha na kuwaza kurejea nchini.

“Tamthilia ni ya kisasa zaidi kwani lengo letu pia ni kuonyeshwa nje ya nchi na kuonyesha madhari ya kuvutia ya jiji letu la Dar es Salaam na kupromoti mji wetu tofauti na hali iliyozoeleka kwani tamthilia nyingi uonyesha maisha ya vijijini,” alisema Johnson.

Alifafanua kuwa kwa kuonyesha usafi wa mji, maeneo mbalimbali ya starehe ya hapa nchini, kutawavutia hata wasanii watayarishaji wa tamthilia nje ya nchi kuja kutayarishia kazi zao hapa nchini.

Alisema kuwa tamthilia hiyo ina jumla ya sehemu 12 ambapo katika kila sehemu, muigizaji mkuu ma maudhui ya tamthilia pia yanabadilika.

No comments: